Watu wanne wa familia ya Kiislamu wameuawa "kimakusudi" katika shambulio la gari siku ya Jumapili, polisi wa Canada wanasema.
Shambulio hilo lilitokea katika mji wa London, mkoa wa Ontario. Mvulana wa miaka tisa, wa familia hiyo aliyenusurika amelazwa hospitali akiwa na majeraha mabaya.
Mwanamume wa miaka 20 raia wa Canada amefunguliwa mashtaka manne ya jaribio la mauaji.
Shambulio hilo lilikuwa baya zaidi kufanywa dhidi ya jamii ya Waislamu wa Canada tangu watu sita walipouawa katika msikiti mmoja mjini Quebec mwaka 2017.
"Inaaminiwa wahasiriwa walilengwa kwa sababu walikuwa Waislamu," Det Supt Paul Waight aliwaambia waandishi wa habari siku ya Jumatatu.
Polisi wanatafakari uwezekano wa kufungua mashtaka ya ugaidi, alisema, akiongeza inaaminiwa kuwa uhalifu wa chuki.
Tunafahamu nini?
Wahasiriwa ni wanawake wawili- walio na umri wa 74 na 44 - mwanamume wa miaka 46-na msichana wa miaka 15. Majina yao hayajatolewa kufuatia ombi la familia. Mvulana wa miaka tisa yuko hospitali baada ya kujeruhiwa katika shambulio hilo, polisi walisema.
Polisi wamemtaja mtuhumiwa ni Nathanial Veltman, 20, wa London, Ontario. Alikamatwa bila visa vyo vyote vya ghasia karibu kilomita sita kutoka eneo la tukio.
Bado haijabainishwa ikiwa mshukiwa ana uhusiano na makundi yoyote ya chuki, alisema Det Supt Waight.
Kumbukumbu ya muda mfupi kwa wahasiriwa iliwekwa katika eneo la shambulio hilo
Wakaazi wengi waligutushwa baada ya shambulio hilo
"Hakuna uhusiano wowote wa hapo awali kati ya mtuhumiwa na wahasiriwa," Det Supt Waight alisema, akiongeza kuwa mtuhumiwa alikuwa amevalia fulana ambayo inaonekana kama "nguo ya kujikinga mwili".
Polisi wanasema Bw. Veltman hajawahi kushtakiwa siku zilizopita.
Mmoja wa mashuhuda aliaimbia CTV News kwamba alimfumba macho binti yake mdogo asione miili ya wahasiriwa.
Mwingine aliimbia CTV kwamba hali katika eneo hilo ilikuwa ya "taharuki".
"Watu walionekana wakikimbia kila mahali anaokimbia," alisema Paige Martin. "Raia walikuwa wakijaribu kuelekeza magari ya huduma za dharura pakwenda."
Sensa ya mwaka 2016 ilibaini kuwa London - mji uliopo karibu kilo mita 200 kusini magharibi mwa mwa Toronto - unaendelea kuwa na watu kutoka jamii mbali mali. Mmoja wa watu watano alizaliwa nje ya Canada, Waarabu ndio jamii kubwa ya wachache, wakifuatiwa na jamii kutoa Asia Kusini.
Shambulio hilo limepokelewaje?
Waziri Mkuu wa Canada Justin Trudeau aliandika katika Twitter yake akisema ilikuwa taarifa ya "kuogofya".
"Kwa wapendwa wa wale ambao walitishwa na kitendo cha jana cha chuki, tuko hapa kwa ajili yenu," aliandika.
Mwisho wa Twitter ujumbe, 1
Mwisho wa Twitter ujumbe, 2
"Hiki kilikuwa kitendo cha mauaji ya watu wengi, kilichotekelezwa dhidi ya Waislamu, dhidi ya wakazi wa London, kilichotokana na chuki," alisema Meya wa London Ed Holder.
Katika taarifa, Meya Holder alisema anazungumza na "kwa niaba ya wakazi wote wa London ninaposema nyoyo zetu zimevunjika".
"Tunaomboleza familia, vizazi vitatu ambavyo sasa vimekufa."
Taarifa ya Meya iliongeza kuwa ameagiza bendera zote kupeperushwa nusu mlingoti nje ya ofisi za baraza la jiji la London kwa ajili ya maombolezo ya siku tatu.
Polisi wanaamini wahasiriwa walilengwa kwasababu ya imani yao




