Kijana wakipalestina aliyepigwa risasi na wanajeshi wa Israel afariki dunia
Wizara ya afya ya mamlaka ya Wapalestina imesema mvulana wa Kipalestina aliyepigwa risasi na wanajeshi wa Israel katika Ukingo wa Magharibi jana, amefariki kutokana na majeraha yake. Jeshi la Israel lilisema jana Jumatano kwamba mwanajeshi aliewekwa karibu na kituo cha walowezi karibu na mji wa Ukingo wa Magharibi wa Neblus, alimpiga risasi kijana huyo Ahmad Shamsa mwenye umri wa miaka 15, baada ya kurusha kitu cha mashaka kilicholipuka mbele yake. Mapema hapo jana, jeshi la Israel lilimpiga risasi na kumuua mwanamke wa Kipalestina, kwa madai kwamba alijaribu kuwagonga kwa gari, kundi la wanajeshi wanaolinda kituo cha ujenzi katika Ukingo wa Magharibi. Mashirika ya haki za binadamu ya Palestina na Israel, yanalishtumu jeshi la Israel kwa kutumia nguvu kupita kiasi, dhidi ya Wapalestina wanaofanya mashambulizi ya visu na mawe, waliosema wanaweza kudhibitiwa bila kuuwawa.

