Waziri wa Afya nchini Tanzania imeanza kutoa takwimu ya watu walioambukizwa virusi vya corona, kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini humo.
Waziri wa Afya Dkt Dorothy Gwajima amenukuliwa kusema hadi kufikia Julai 8, 2021 jumla watu 408 wamebainika kuwa na ugonjwa wa corona huku 284 wakitumia mitungi ya oksijeni.
Kulingana na Gazeti la Mwananchi Dkt Gwajima alitoa taarifa hiyo leo Jumamosi wakati akitoa elimu ya kujikinga na ugonjwa huo jijini Dodoma.
Hatua hii ya hivi punde inatilia mkazo juhudi ya Tanzania katika vita dhidi ya Covid-19.
Rais Samia amesema nini kuhusu Covid?
Rais Samia Suluhu Hassan mara kwa mara amekuwa akiwakumbusha Watanzania kuendelea kuchukua tahadhari na kujilinda dhidi ya wimbi la tatu la janga la corona.
Rais Samia Suluhu alichukua uongozi Machi mwaka huu
Katika moja ya ziara yake akiwa njiani kutoka Dodoma Rais Samia alielezea kushangaa kuona mamia ya watu bila barakoa
Alitaja miji ya Kagera, Arusha, Mwanza, Dar es Salaam kuwa maeneo ya yaliyo na idadi ya juu ya wagonjwa wa Corona.
Alisisitiza hitaji la kila mtu kuwajibika katika nyakati hizi za kujaribu wakati ulimwengu wote unapambana na shida janga hilo la kiafya.
Rais amechukua hatua gani?
Alipochukua uongozi, Rais Samia aliunda kamati ya ushauri kuhusu Covid-19 ambayo iliwasilisha mapendekezo yake kati kati ya mwezi Mei.
Iliishauri serikali kutambua uwezo wa virusi hivyo Tanzania hadharani, kutangaza takwimu kuhusu Covid-19 kwa umma na kuziwasilisha pia kwa Shirika la Afya Duniani (WHO).
Aidha, iliishauri serikali kujiunga na mpango wa kiamataifa wa kutoa chanjo unaoungwa mkono na Umoja wa Mataifa wa Covax.
Siku za mwanzo baada ya kuchukua uongozi, Rais Samia mwenyewe alikuwa akitokea kadharani bila barakoa.
Alivalia barakoa katika safari zake nje ya nchi Uganda na Kenya, lakini alikuwa akirejea Tanzania bila kuvalia barakoa.
Lakini siku za karibuni, amekuwa akivalia sana barakoa na kuwahimiza Watanzania kuvalia barakoa pia.
Idara za serikali pia zimekuwa zikiwahimiza raia kuvaa barakoa.
Na sasa kumetolewa mwongozo mpya kuhusu kufunguliwa kwa shule na taasisi nyingine za mafunzo, ambapo ni pamoja na kuvaliwa kwa barakoa, watu kutokaribiana, kuwepo vituo vya watu kunawa mikono na pia kuwepo kwa vitakasa mikono.


