Iran yafanya uchaguzi wa urais
Iran inafanya uchaguzi wa urais hii leo huku jaji mwenye msimamo mkali Ebrahim Raisi akitarajiwa pakubwa kushinda na kumrithi Rais Hassan Rouhani. Hata hivyo wengi hawatarajiwi kushiriki uchaguzi huo kutokana na hali ngumu ya kiuchumi iliyochangiwa na vikwazo vya kiuchumi vya Marekani pamoja na miito ya kususia uchaguzi huo iliyotolewa na wafuasi wa uliberali kutoka ndani na nje ya Iran. Mapema leo kiongozi wa juu wa taifa hilo Ayatollah Ali Khamenei amepiga kura yake huku akiwaomba watu kujitokeza, huku akisema kila kura ina umuhimu kwao na kimataifa. Utafiti wa maoni umeashiria idadi ya watakaojitokeza kufikia asilimia 44 kati ya watu milioni 59 wanaostahili kupiga kura.
