Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema anataka kukuza ushirikiano katika masuala yenye maslahi ya pamoja katika mkutano wake na mwenzake wa Marekani, Joe Biden.Amesema hayo katika mahojiano yake na televisheni ya umma ya nchini mwake ambayo yamerushwa leo. Rais Putin amesema ana maanisha kwamba, kuna masuala ambayo wanaweza kuyafanyia kazi kwa ufanisi kama mizozo ya kikanda, wasiwasi wa kimazingira na suala la utulivu wa kimkakati.Mkutano wa kwanza kati ya Marekani na Urusi tangu Biden aingie madarakani utafanyika Jumatano ijayo mjini Geneva, Uswisi. Kuna mvutano mkubwa kati ya pande hizo mbili kuhusu masuala kadhaa kuanzia haki za binaadamu hadi kuingilia uchaguzi, udukuzi na hali jumla ya kuzorota kwa mahusiano kwa wakati huu.
