Urusi kufanya mazungumzo na Marekani kuhusu udhibiti wa silaha
Urusi imesema inatarajia kufanya mazungumzo na Marekani kuhusu udhibiti wa silaha katika wiki chache zijazo baada ya kukubaliana kufanya hivyo katika mkutano wa kilele wa Geneva. Naibu waziri wa mambo ya nje wa Urusi amesema hayo katika majadiliano yaliyochapishwa leo kwenye tovuti ya wizara yake. Rais wa Marekani Joe Biden na wa Urusi Vladimir Putin wamekubaliana katika mkutano wa kilele wa Geneva hapo jana kuanza mazungumzo hayo ya kimkakati ili kuweka misingi ya kudhibiti silaha katika siku za usoni. Marais hao wawili walitumia zaidi ya masaa matatu kujadili maswala tofauti ikiwa ni pamoja na kurudisha mabalozi wao mjini Moscow na Washington ili kuimarisha uhusiano wao wakidiplomasia ulioharibika.

