Viongozi wakuu wa China na Urusi waongeza ushirikiano wa kirafiki na ujirani mwema
Viongozi wakuu wa China na Urusi wamekubaliana kurefusha rasimu ya makubaliano ya ujirani mwema na ushirikiano wa kirafiki. Kwa mujibu wa shirika la habari la serikali ya China, Xinhua, hatua hiyo imefikiwa leo wakati wa mazungumzo yaliyofanyika katika mkutano wa kilele kwa njia ya vidio kati ya marais Xi Jinping na Vladmir Putin. Katika mkutano huo, Putin amesema rasimu hiyo ya makubaliano ya msingi ya kuungana mkono katika kulinda mshikamano wa madola yao na uthabiti katika maeneo yao ni muhimu sana katika ulimwengu wa sasa. Urusi inaiuzia China mafuta, gesi na mkaa wa mawe wakati nchi hiyo yenye idadi kubwa ya watu duniani ikiiuzia Urusi mashine na bidhaa nyingine. Nchi zote mbili mara nyingi husimamia maslahi sawa katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
