Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan kuvilipa vyombo vya habari ambavyo vinadai zaidi ya Sh6 bilioni sambamba na Serikali kutangaza kwenye vyombo vya habari binafsi.
Balile amewasilisha ombi hilo leo Jumatatu Juni 28, 2021 Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano wa Rais Samia na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari kuzungumzia siku 100 za uongozi wa Samia tangu alipoapishwa kuwa kiongozi mkuu wa nchi Machi 19, 2021.
Amesema Waziri Mkuu, Kassimu Majaliwa alipohudhuria mkutano mkuu wa TEF mjini Morogoro, aliahidi kushughulikia malipo ya vyombo hivyo kabla ya Juni 30, 2021 na kwamba wataendelea kufanya kazi na vyombo vyote vya habari.
“Hali ya uchumi ya vyombo vya habari ni mbaya, magazeti mengi yamejifunga yenyewe kwa sababu ya hali ngumu kifedha kwa sababu kulikuwa na tangazo la chini chini kwamba Serikali isitangaze kwenye vyombo binafsi na kampuni nane zinaidai serikali zaidi ya Sh6 bilioni.”
“Tunaomba uongeze nguvu kwenye uamuzi wa Waziri Mkuu wa kuvilipa vyombo hivi lakini tunaomba ufute uamuzi wa kutotangaza kwenye vyombo binafsi,” amesema Balile wakati akitoa neno la utangulizi.
Ameitaka Serikali kuweka vichocheo vya kiuchumi kwenye vyombo vya habari ili viweze kujiendesha kwa weledi.
“Nchi za wenzetu wameweka stimulus kidogo kwenye sekta ya habari, tunakuomba ikikupendeza uliangalie hilo pia,” amesema Balile.
Vilevile, amezungumzia sheria ya huduma za habari akisema imeanzisha vyombo vinne ambavyo ni idara ya habari maelezo, baraza huru la vyombo vya habari, jambo ambalo anaona ni udhibiti mkubwa wa vyombo vya habari badala ya kuviwezesha.
